Sudan : Mapigano yanaendelea kusambaa katika maeneo zaidi
Nairobi – Vita vinavyoendelea kati ya wanajeshi na wanagambo wa RSF nchini Sudan, vinaendelea kusambaa katika maeneo ambayo yamekuwa yakishuhudia utulivu, wakati huu raia wengi wa jimbo la Darfur wakiendelea kuyakimbia makaazi yao.
Imechapishwa:
Wakaazi wa maeneo ya Kusini mwa Sudan wanasema tangu siku ya Alhamisi, makabiliano makali yamekuwa yakishuhudiwa katika mji wa El Fasher ambao umekuwa na utulivu kwa miezi miwili baada ya kuzuka kwa mapigano hayo Aprili 15.
Hali kama hiyo pia inashuhudiwa pia katika jimbo la Kordfan Kaskazini, wakati huu shughuli za usafiri zikitatizwa katika baadhi ya maeneo ya jiji kuu la Khartoum.
Vita hivyo vimesababisha watu zaidi ya laki sita, kutoka jimbo la Darfur kukimbilia katika mji wa El Fasher, huku wengine wakikimbilia katika nchi jirani kama Chad.
Katika hatua nyingine, kundi la waasi la Tamazuj Front lililotia saini mkataba wa amani, limetanagza kujiunga na wanamgambo wa RSF, wakati huu kukiwa hakuna dalili ya vita hivyo ambavyo vimesababisha vifo vya zaidi ya watu elfu nne kufika mwisho.