Wakuu wa kijeshi wa nchi za Ecowas kukutana kujadili Niger
Nairobi – Vyanzo vya kijeshi vinasema wakuu wa jeshi kutoka nchi za Jumuiya ya Afrika Magharibi (ECOWAS) watakutana nchini Ghana siku ya Alhamis na Ijuma kujadili uwezekano wa kutumia nguvu za kijeshi nchini Niger.
Imechapishwa:
Mkutano huo uliratibiwa kufanyika baada ya viongozi wa Ecowas kuagiza kuekwa tayari kwa jeshi kuingilia kati kuhusu kinachoendelea nchini Niger na kurejesha utawala wa kiraia baada ya kuangushwa kwa uongozi wa rais Bazoum tarehe 26 ya mwezi Julai.
Kikao hicho kilikuwa kimepangwa kufanyika Jumamosi jijini Accra kabla ya kuhairishwa hadi wiki hii wakati huu Ecowas ikiwa inaendelea kujadiliana na mkuu wa utawala wa kijeshi jijini Niamey Abdourahmane Tchiani.
Wakuu wa Ecowas walikutana katika mji wa Abuja nchini Nigeria Alhamis iliyopita ambapo walisisitiza malengo ya Jumuiya hiyo kutumia njia za kideplomasia kuhusu kinachoendelea Niger.
Niger, taifa ambalo halina bahari katika ukanda wa Sahel, ni mojawapo ya mataifa maskini zaidi duniani, likiwa pia linakabiliwa na utovu wa usalama.
Bazoum, mwenye umri wa miaka 63, aliponea mapinduzi mawili ya kijeshi kabla ya kuangushwa baadae katika mapinduzi ya tano katika historia ya taifa hilo.