Niger yatangaziwa vikwazo zaidi baada ya kukataa kukutana na ECOWAS
Nchi ya Niger imetangaziwa vikwazo zaidi baada ya viongozi wa mapinduzi nchini humo kukataa kukutana na ujumbe wa ECOWAS kwa mazungumzo ya kurejesha utawala wa kiraia.
Imechapishwa:
Rais wa Nigeria ambaye pia ndiye mwenyekiti wa ECOWAS, ameagiza benki kuu ya ya nchi yake kufunga akaunti za benki za wote ambao wamehusika kwa mapinduzi nchini Niger.
Ni hatua inayokuja baada ya uongozi wa kijeshi nchini Niger kukataa kukutana na ujumbe wa ECOWAS na wale wa umoja wa mataifa ambao walilenga kufanya mazungumazo ya kumrejesha rais Mohamed Bazoum madarakani.
Baadaye leo wakuu wa mataifa ya ECOWAS wanatarajiwa kukutana kujadili hatua gani zitachukuliwa baada ya uongozi wa kijeshi kupuuza maktaa ya ecowas ya kurejesha utawala wa kiraia siku ya jumapili.
Tayari viongozi wa kijeshi wa Ecowas wamesema wako tayari kutumia nguvu iwapo wataangizwa kufanya hivyo.
Haya yanajiri wakati huu Marekani imesema inajaribu kuzuia kundi la wapiganaji mamluki wa Urusi, Wagner, kutumia mapinduzi ya nchini Niger kujipenyeza zaidi kwenye ukanda huo, licha ya juhudi zake za juma hili kugonga ukuta.
Akizungumza na shirika la utangazaji la Uingereza, waziri wa mambo ya nje wa Marekani, Antony Blinken, amesema wanaguswa na taarifa kuwa watawala wa kijeshi wameomba ushirikiano na kundi hilo.
‘‘Tunaguswa haswa pale tunapoona kundi kama Wagner kukua katika maeneo tofauti ya ukanda wa Sahel.’’ amesema Antony Blinken.
Antony Blinken kuhusu Niger
Blinken, aidha ameeleza kuwa wanaguswa na suala hilo kwa sababu kila eneo ambalo kundi hilo limeenda, vifo, uharibifu na uporaji wa mali.
Kiongozi huyo vilevile amesema kinachoendelea nchini Niger huenda kinachochewa na kundi la Wagner lakini wanajiribu kutumia mwanya huu kama ilivyotokea kwenye nchi kadhaa.