ECOWAS kufanya kikao mjini Abuja kujadili Niger
Nairobi – Viongozi wa nchi za ukanda wa Afrika Magharibi, juma hili wanatarajiwa kukutana tena mjini Abuja, Nigeria kujadili hatua zaidi za kuchukua dhidi ya Niger, baada ya wanajeshi kukaidi makataa ya kuvamiwa kijeshi ikiwa hawataurejesha utawala wa rais Mohamed Bazoum.
Imechapishwa:
Cheza - 00:48
Mkutano huu unaenda kufanyika wakati ambapo Italia ikitoa wito kwa ECOWAS kuongeza muda wa mazungumzo na wanajeshi.
Taarifa za mkutano wa wakuu wa nchi za ECOWAS ni ya kwanza kutolewa na jumuiya hiyo, tangu kumalizika kwa muda wa mwisho waliotoa kwa jeshi kurejesha utawala wa kiraia ama waondolewe kwa nguvu.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na ECOWAS, viongozoi hao watakutana Alhamisi ya wiki hii kujadiliana na kutathmini hali ya kisiasa kwenye taifa hilo, wakati huu mwito wa majadiliano zaidi na wanajeshi ukiendelea kutolewa.
Licha ya muda wa mwisho uliotolewa na jumuiya hiyo kutamatika siku ya Jumapili, hakukuwa na tangazo lolote la kutumwa kwa wanajeshi wa kigeni, ambapo jeshi la Niamey lilionya kujibu uvamizi wowote wa nchi za ukanda.
Haya yanajiri wakati huu Mali na Burkina faso, ambazo zimesimamishwa uanachama wa ECOWAS zikisema zinatuma ujumbe maalumu nchini Niger, kuonesha mshikamano na taifa hilo.