Ufaransa inaitika Niger kuhakikisha ubalozi wake unalindwa
Nairobi – Wizara ya mambo ya kigeni ya Ufaransa, imewataka viongozi wa mapinduzi ya kijeshi nchini Niger kuhakikisha wanatoa usalama kikamilifu kwenye ubalozi wake mjini Niamey.
Imechapishwa:
Wito wa Paris unakuja wakati huu maandamano zaidi yakitarajiwa kufanyika nchini humo ambapo hadi tukichapisha taarifa hii, waandamanaji walikuwa wameanza kukusanyika katika mji mkuu wa taifa hilo.
Jumamosi iliyopita, waandamanaji walishambulia ubalozi wa Ufaransa nchini humo hatua ambayo iliilazimu Paris kuwaondoa raia wake nchini Niger.
Waanadmanaji wanaounga mkono mapinduzi ya kijeshi wamekuwa wakitaka wanajeshi wa Ufaransa na wale wa Marekani kuondoka kwenye taifa hilo la Afrika Magharibi.
Washington imewataka wafanyikazi wake ambao hawafanyikazi katika sekta za dharura kuodoka na kutoa wito wa raia wake kutosafiri kuelekea nchini Niger.
Rais wa Marekani, Joe Biden ametoa wito wa kuachiwa kwa haraka rais anayezuiliwa na jeshi nchini Niger Mohamed Bazoum.