Niger: AU inawapa wanajeshi siku kumi na tano 'kurudi kambini mara moja'
Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika (AU) linawataka wanajeshi waliofanya mapinduzi nchini Niger kurudi kambini mara moja na bila masharti na kurejesha mamlaka ya kikatiba, ndani ya muda wa siku kumi na tano.
Imechapishwa:
Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika (AU) limeyasema hayo katika taarifa kwa vyombo vya habari iliyochapishwa baada ya mkutano, Ijumaa, Julai 28, kufuatia mapinduzi dhidi ya Rais Mohamed Bazoum.
Wakati huo huo Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limelaani vikali hatua ya kubadilishwa kwa serikali halali ya Niger kwa kukiuka katiba, na kutoa wito wa kuachiliwa huru mara moja kwa Rais wa nchi hiyo Mohammed Bazoum.
Katika taarifa iliyokubaliwa kwa pamoja, baraza hilo lenye wanachama 15 lilisisitiza haja ya kumlinda Bazoum, familia yake na maafisa wa serikali yake.
Hayo yanajiri wakati Marekani imetoa "uungaji mkono wake usio na kikomo" kwa rais aliyepinduliwa nchini Niger Mohamed Bazoum.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken alionya wale wanaomzuilia Bw Bazoum kwamba "mamilioni ya dola za msaada" ziko hatarini.
Bw Bazoum aliondolewa katika mapinduzi wiki hii yaliyoongozwa na Jenerali Abdourahmane Tchiani, anayejulikana pia kama Omar Tchiani, mkuu wa kitengo cha walinzi wa rais.