UN yaonya kuhusu madhara ya vita vinavyoendelea nchini Sudan
Umoja wa Mataifa, unaonya kuwa vita vinavyoendelea nchini Sudan kati ya wanajeshi na wanamgambo wa RSF yanatishia kugeuka kuwa ya wenyewe kwa wenyewe, yanayoweza kutikisa nchi za ukanda.
Imechapishwa:
Onyo hili limetolewa baada ya ndege za kijeshi, kushambulia makaazi ya watu na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 20.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres, amelaani shambulio hilo lilitokea kwenye mji wa Omdurman, ambaye ameongeza kuwa iwapo vita vinavyoendelea havitakoma, ukanda mzima upo kwenye hatari ya kuathiriwa.
Imepita sasa miezi tatu tangu kuanza kwa mapigano hayo na juhudi za Kimataifa kujaribu kuzileta pamoja, pande mbili zinazopigana, vimeambulia patupu.
Mpaka sasa watu zaidi ya 3,000 wameuawa kwenye mzozo huu, huku kukiwa na ripoti za wanawake na wasichana kubakwa. Umoja wa Mataifa unaonya kuwa visa vya uhalifu wa kivita, vinaendelea katika jimbo la Darfur.
Wanamgambo wa RSF wamejenga kambi zao katika makaazi ya watu na kusababisha raia wa kawaida kuyakimbia makaazi yao, wakati huu takwimu za Umoja wa Mataifa zikieleza kuwa watu 3,000,000 wameyakimbia makwao, wakiwemo 700,000 waliokimbilia kwenye nchi jirani.