Raia wa CAR wametoa wito kwa ICC kuongeza mashtaka dhidi ya Joseph Kony
Nairobi – Raia wa Jamhuri ya Afrika ya kati wamemtaka mwendesha mashtaka wa Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa Kivita ICC, kuongeza mashtaka zaidi dhidi ya kiongozi wa kundi la Lord's Resistance Army LRA, Joseph Kony Kufuatia kile kinachoelezwa kuwa wapiganaji wake waliokimbilia kwenye nchi yao wameendeleza vitendo vya mauaji na unyanyasaji.
Imechapishwa:
Cheza - 00:38
Katika taarifa yao raia hao wamekumbusha kuwa kiongozi huyo ambaye anasakwa na mahakama ya ICC tangu mwaka wa 2005, anashukiwa kwa dhulma dhidi ya binadamu na uhalifu wa kivita uliofanywa kaskazini mwa Uganda, kabla ya kukimbilia katika misitu ya nchi yao.
Mwaka 2006, kufuatia kushindwa kwa mazungumzo ya amani, wanamgambo hao walihamia Jamhuri ya Afrika ya Kati ambako wanaendelea kufanya vitendo vya uhalifu ikiwemo mauaji na ubakaji dhidi ya wanawake, na sasa wameitaka mahakama ya ICC kuharakisha mchakato wa kisheria ili akamatwe.
Taarifa hii inakuja baada ya mwezi Desemba mwaka jana Mahakama ya ICC, kutupilia mbali rufaa ya Dominic Ongwen, ambaye alitaka imuachie kwakuwa alijiunga na kundi la Joseph Kony akiwa mtoto.