UN yalaani unyanyasaji wa kimapenzi dhidi ya wanawake nchini Sudan
Umoja wa Mataifa umelaani ongezeko la visa vya unyanyasaji wa kimapenzi dhidi ya wanawake na wasichana nchini Sudan, wakati huu mapigano yakiendelea kati ya jeshi la taifa na wanamgambo wa RSF.
Imechapishwa:
Tume ya haki za binadamu ya Umoja huo inasema, wanawake na wasichana 57 wamebakwa katika matukio 21 tangu kuanza kwa vita hivyo, wakati huu pia Shirika la afya duniani WHO likitoa wito kwa wanawake na wasichana kupata huduma za afya.
Jeshi limekuwa katika vita na kikosi cha wanamgambo wa RSF katika mapigano ambayo yameua karibu watu 3,000 na mamilioni ya wengine kuyahama makazi yao. Tedros Ghebreyesus ni Mkurugenzi Mkuu wa WHO.
“Machafuko yanayoendelea ikiwa ni pamoja na kuwashambulia wahudumu wa afya na vituo vya kutoa huduma, yanazuia wagonjwa kupata huduma muhumu.” amesema Tedros Ghebreyesus ni Mkurugenzi Mkuu wa WHO.
Tedros Ghebreyesus, Mkurugenzi Mkuu wa WHO
Aidha mkuu huyo wa WHO ameeleza kuwa wanawake na wasichana wanapaswa kupata huduma wanzohitaji haswa wanapotia changamoto hizo za dhuluma za kimapenzi.
Vita vinavyoendelea vimesababisha kufungwa kwa hospitali zaidi ya 60.
Mapigano hayo yamesababisha idadi kubwa ya raia wa Sudan kukabiliwa na ukosefu wa chakula na uhaba dawa wakati huu wito ukiendelea kutolewa kwa pande hasimu kusitisha mapigano.