Rais wa Kenya awafuta kazi maafisa wa afya baada ya sakata ya ulaghai wa vyandarua
Nairobi – Rais wa Kenya William Ruto amemfuta kazi katibu mkuu anayesimamia afya ya umma na kuvunja bodi nzima ya taasisi ya kununua vifaa vya matibabu kutokana na kashfa ya ufisadi.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kisa hicho kinahusisha zabuni ya usambazaji wa vyandarua vya thamani ya takribani dola milioni 27 vilivyotolewa na wafadhili kwa lengo la kukabiliana na mbu wanaosababisha malaria.
Hazina ya Global Fund ilikuwa imeagiza Mamlaka ya Ugavi wa Dawa nchini (Kemsa) kununua zaidi ya vyandarua milioni 10 ambavyo vingetolewa kwa watu walio na mapato ya chini katika kaunti kadhaa zinazokabiliwa na ugonjwa wa malaria.
Lakini Global Fund ilighairi zabuni hiyo ikishutumu Kemsa kwa makosa ya kudaiwa kupendelea kampuni moja ambayo nyaraka zake hazikuwa katika mpangilio na kuwafungia nje wengine.
Mnamo 2020, Kemsa iliangaziwa tena kutokana na madai ya matumizi mabaya ya mamilioni ya dola yaliyokusudiwa kununua vifaa vya kinga wakati wa janga la Covid.kesi ambayo mpaka sasa inasikilizwa.
Tathmini ya Malaria nchini Kenya imeyatenga maeneo ya Siaya,Kisumu, Migori,Homa bay,Vihiga,Bungoma na Busia kuwa yale yanayotatizwa zaidi na malaria kwenye eneo la kanda ya Ziwa.Ya pwani ni pamoja na Mombasa, Kilifi, Kwale,Lamu na Taita Taveta.Kutokana na tathmini hiyo, serikali ilizindua mwaka 2019 chanjo ya Malaria mahsusi kwa watoto wadogo. Ugonjwa wa malaria ni moja ya vyanzo vya maafa kwa watoto wadogo hasa walio na umri wa chini ya miaka 5.