Sudan Kusini yawapokea zaidi ya raia elfu kumi wanaokimbia mapigano Sudan
NAIROBI – Mapigano nchini Sudan yameingia wiki ya pili bila kuonekana mwanga wa kupata suluhisho na kusitisha mapigano kati ya majenerali wawili.
Imechapishwa:
Takriban raia elfu kumi wamekimbilia usalama wao nchini Sudan Kusini katika siku za hivi maajuzi.
Siku ya Jumatatu, Aprili 24, kamishna wa jimbo la Renk, nchini Sudan Kusini, Kak Padiet, amekiambia chombo cha habari cha Reuters kuwa karibia raia elfu sita na mia tano walivuka mpaka siku ya Jumamosi huku wengine elfu tatu wakivuka siku ya Jumapili.
Raia wengine wanaokimbia mapigano hayo wanatarajiwa kuvuka na kuingia Sudan Kusini siku ya Jumatatu, Aprili 24.
Kwa upande wake kamanda wa jeshi wa Renk, Dau Aturjong, amesema robo tatu ya waliowasili ni raia wa Sudan kusini, na idadi iliyosalia ni raia kutoka Sudan, Eritrea, Kenya, Uganda na Somali.
Kwa sasa shughuli hii ya msaada inafanywa na mamlaka za eneo hilo, mashirika ya misaada bado hayajaingilia kati. Aturjong ameiambia Reuters.
Nchi ya Sudan inawahifadhi wakimbizi laki nane kutoka Sudan kusini, ambao walikuwa wamekimbia mzozo wa muda mrefu nchini humo.
Nchi zawahamisha raia wao
Mapigano haya nchini Sudan kati ya jeshi la Sudan linaloongozwa na jenerali Abdel Fattah al-Burhan na kiongozi wa kikosi cha Rapid Support Forces, RSF, Mohammed Hamdan Daglo, yamezifanya mataifa mbalimbali kuendeleza operesheni ya kuwahamisha raia wake kupitia angani, majini na hata barabarani.
Baadhi ya nchi pia zimesitisha kwa shughuli katika balozi zake nchini humo.
Uwanja mkuu wa ndege wa Khartoum, umekuwa eneo la mapigano makali huku kukiwa na madai kuwa unadhibitiwa na kikosi cha RSF.