Zaidi ya watu 10 wamelazwa nchini Burundi kutokana na mlipuko wa Kipindupindu
Mamlaka za afya nchini Burundi, hapo jana ilitangaza kuwepo kwa mlipuko wa ugonjwa wa Kipindupindu katika jiji la Bujumbura, wagonjwa zaidi ya 10 wakiripotiwa kulazwa hospitalini.
Imechapishwa:
Katika taarifa yake, waziri wa afya Sylvie Nzeyimana, amesema sampuli ambazo zilichukuliwa kwa uchunguzi na majibu kutolewa Jumamosi iliyopita, zimeonyesha kuwepo kwa viini vinavyosababisha kipindupindu.
Maambukizi yameripotiwa katika maeneo ya Bukirasazi, Mutakura na Buyenzi, na yanakuja kipindi hiki ambacho mji wa Bujumbura na viunga vyake inashuhudia mvua kubwa zilizosababisha vyoo kujaa.
Nzeyimana amesema tayari serikali imechukua hatua kudhibiti mlipuko huo ikiwemo kunyunyiza dawa katika makazi ya watu, kuhamasisha jamii na kuwatafuta watu zaidi walioathirika.
Kwa mujibu shirika la madaktari wasio na mipaka, MSF, kipindupindu huathiri kati ya watu 200 hadi 250 kila mwaka nchini Burundi.