Raia wa Afrika Kusini wasubiri mshindi wa uchaguzi wa rais wa chama cha ANC
Nchini Afrika Kusini, matokeo ya kumfahamu rais wa chama tawala cha ANC, yanasubiriwa, baada ya wajumbe zaidi ya Elfu nne, kupiga kura Jumapili iliyopita, huku ushindani mkali ukielezwa kuwa kati ya rais Cyril Ramaphosa na waziri wake wa zamani wa afya Zweli Mkhize.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Licha ushindani huo, ripoti zinasema Ramaphosa, mwenye umri wa miaka 70, anatarajiwa kuthibitishwa katika jukumu litakalofungua njia ya kuwa mkuu wa nchi kwa muhula wa pili, licha ya kashfa mbaya ya wizi wa pesa za umma na upinzani mkali wa ndani.
Lakini kinyang'anyiro hicho kilionekana kuwa karibu zaidi kuliko ilivyotarajiwa hapo awali Jumapili, huku ripoti za wajumbe wa chama kutoka majimbo kadhaa wakibadilisha msimamo wao na kumuunga mkono Mkhize, ambaye Ramaphosa alimfuta kazi wakati wa janga la Uviko 19 kwa madai ya ubadhirifu unaohusisha fedha za kukabiliana na maambukizi.
Zaidi ya wajumbe 4,000 walikuwa wakipiga kura zao kuwachagua maafisa wa nafasi saba za juu za uongozi, ikiwa ni pamoja na rais wa chama, naibu rais, mwenyekiti na katibu mkuu, katika mkutano uliofanyika karibu na Johannesburg.
Chama cha African National Congress (ANC) kiliundwa na Nelson Mandela ili kuongoza mapambano ya kukomesha ubaguzi wa rangi. Baada ya takriban miongo mitatu madarakani, mifarakano katika chama inazidi kuongezeka na uungwaji mkono wao unapungua.