Charles Blé Goudé arejea nyumbani baada ya kesi yake kufutwa ICC
Nchini Cote d'Ivoire, aliyekuwa Waziri na mshirika wa karibu wa rais wa zamani Laurent Gbagbo, Charles Blé Goudé, amererejea nyumbani leo, baada ya kufutiwa kesi ya uhalifu wa kivita iliyokuwa inamkabili katika Mahakama ya Kimataifa ya ICC.
Imechapishwa:
Kiongozi huyo wa zamani wa vuguvugu la vijana katika chama tawala wakati wa utawala wa Gbagbo, kabla ya kurejea kwake nyumbani, alisema hakutaka mapokezi makubwa, akitokea jijini Hague nchini Uholanzi alikokuwa anaishi, kufuatia mashtaka yaliyikuwa yanamkabili, kufuatia machafuko ya baada ya uchaguzi wa mwaka 2010.
Anarejea nyumbani kufuatia serikali nchini humo kutanagza mchakato wa maridhiano ya kitaifa, na kurudi kwake kunakuja pia baada ya majadiliano kati ya viongozi wa nchi hiyo, wakiongozwa na washirika wa karibu wa rais Alassane Ouattara.
Mwanasiasa huyo amepangiwa kukutana na wafuasi wake zaidi ya Elfu tano katika mji wa Yopougon katika tafrija ya kumpokea.
Baada ya machafuko ya baada ya uchaguzi wa mwaka 2010, Ble Goude alikimbilia nchini Ghana lakini akakamatwa mwaka 2014 na kupelekwa Hague alikofunguliwa mashtaka ya uhalfu dhidi ya binadamu, lakini kesi yake ikafutwa mwaka 2019.