Misri yamwalika rais Lula kwenye mkutano wa COP27
Misri, ambayo inajiandaa kuwa mwenyeji wa mkutano wa kilele wa Umoja wa Mataifa kuhusu hali ya hewa, COP27, imealika miongoni mwa wakuu wa nchi wanaotarajiwa, rais mteule wa Brazil Luiz Inacio Lula da Silva, aliyechaguliwa hivi karibuni kuchukua nafasi ya Jair Bolsonaro, ambaye rekodi yake ya mazingira inachukuliwa kuwa mbaya.
Imechapishwa:
Msemaji wa Lula ameliambia shirika la habari,la AFP siku ya Jumanne kwamba rais, aliyechaguliwa siku ya Jumapili, "anakifikiria kuhudhuria mkutano wa kilele wa Umoja wa Mataifa kuhusu hali ya hewa, COP27", lakini "bado alikuwa hajachukuwa uamuzi".
"Rais Abdel Fattah al-Sissi anampongeza Rais Lula da Silva kwa kuchaguliwa kwake (...) na kumwalika kuhudhuria mkutano wa kilele wa Umoja wa Mataifa kuhusu hali ya hewa, COP27," imesema taarifa ya msemaji wa rais wa Misri Bassam Radi siku ya Jumatatu.
"Ni hakika kwamba Brazil ina jukumu chanya katika mkutano huu ambao unalenga kuimarisha hatua za hali ya hewa katika ngazi ya kimataifa", taarifa hiyo inaongeza.
Wanaharakati wengi wa hali ya hewa wamesema wanatumai ushindi kutoka kwa Lula ili kuendeleza harakati zao nchini Brazil na kwenye mkutano wa COP27.
Chini ya Rais wa mrengo mkali wa kulia Jair Bolsonaro, ukataji miti wa kila mwaka huko Amazoni umeongezeka kwa wastani wa 75% katika muongo uliopita.
Jumapili, jioni ya kuchaguliwa kwake, Lula alithibitisha kwamba "Brazil iko tayari kurejesha uongozi wake katika mapambano dhidi ya mzozo wa hali ya hewa".
Misri itapokea zaidi ya viongozi 90 wa dunia kuanzia Novemba 6-18, kulingana na waandalizi wa COP27, akiwemo Rais wa Marekani Joe Biden.