Afrika Kusini: Watu 15 wapigwa risasi katika eneo la Soweto.
Polisi nchini Afrika Kusini, imesema watu 19 wameuawa mwishoni mwa juma lililopita, wakati watu wenye silaha waliposhambulia maeneo mawili tofauti ambayo watu walikuwa wakiburudika, tukio ambalo rais Cyril Ramaphosa, amesema halikubaliki.
Imechapishwa:
Polisi kwenye mji wa Soweto, wamesema watu 15 waliuawa katika eneo moja walilokuwa wakipata burudani, ambapo mtu mwenye silaha aliyekuwa katika gari, alifika na kuanza kuwafyatulia risasi.
Katika tukio jingine, polisi kwenye mji wa Pietrmaritzburg, wamethibitisha kuuawa kwa watu wane, baada ya watu wawili waliokuwa na bunduki kuwashambulia wateja waliokuwa katika baa moja.
Aidha polisi kwenye taarifa yao wamesema hadi sasa hakuna watu waliokamtwa kuhusiana na matukio yote mawili, ingawa uchunguzi umeshaanza kubaini wahusika na sababu za mauaji hayo.
Matukio kama haya yamekuwa yakiripotiwa mara kwa mara nchini Afrika Kusini, kutokana na uhasama wa makundi ya kijamii na kusambaa kwa silaha haramu.