ECOWAS yaiondolea Mali vikwazo vya kiuchumi
Jumuiya ya Kiuchumi ya nchi za Afrika Magharibi ECOWAS, imeiondolea Mali, vikwazo vya kiuchumi, baada ya kukubali mpango wa uongozi wa kijeshi kuandaa uchaguzu mkuu mwaka 2024 ili kurejesha uongozi wa kiraia, lakini pia imekubali mpango wa jeshi nchini Burkina Faso kurejesha uongozi wa kiraia baada ya kipindi cha miaka miwili.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Uamuzi huu umechukuliwa na viongozi wa Jumuiya hiyo waliokutana jumapili jijini Accra nchini Ghana, kuthathmini mipango ya nchi za Mali, Guinea na Burkina Faso kurejea kwenye uongozi wa kidemokrasia baada ya jeshi kufanya mapinduzi kwa nyakati tofauti.
Mali ndio ilikuwa nchi ya Kwanza kupinduliwa na jeshi mara mbili mwaka 2020 na 2021, ikafuatwa na Guinea mwaka uliopita na Burkina Faso Januari mwaka huu.
Rais wa Tume ya Jumuiya hiyo, Jean-Claude Kassi Brou, amesema viongozi wa nchi hizo za Afrika Magharibi wamekubali kuindolea Mali vikwazo vya kiuchumi na kulitaka jeshi kutokuwa na mwakilishi katika kinyanganyiro cha urais, wakati uchaguzi utakapofanyika mwaka 2024.
Kuhusu Burkia Faso, ECOWA imekubali mpango wa uongozi wa jeshi kuwa na kura ya maoni kuhusu Katiba mwaka 2024 na baadaye kuandaa uchaguzi wa wabunge na urais mwezi Februari mwaka 2025.
Hata hivyo, hakuna maamuzi yoyote yaliyochukuliwa kuhusu Guinea ambayo, uongozi wa kijeshi umependekeza kusalia madarakani kwa kipindi cha miezi 36 baada ya kukataa kumpokea msuluhishi wa ECOWAS , mapendekezo ambayo yamekataliwa na Umoja wa Afrika.