DRC yaishtumu Rwanda kwa kuvamia mji wa Bunagana
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, sasa inaishtumu Rwanda kwa uvamizi, baada ya waasi wa M 23 kuuteka mji wa Bunagana ulio katika mpaka na Uganda siku ya Jumatatu baada ya mapigano na wanajeshi wa FARDC.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Cheza - 00:14
Jeshi la DRC katika taarifa yake imewashtumu wanajeshi wa Rwanda kwa kuuteka mji huo.
Jenerali Sylvain Ekenge, msemaji wa uongozi wa kijeshi katika jimbo la Kivu Kaskazini amesema, Rwanda imeamua kuuvamia mji huo baada ya kubaini kuwa, waasi wanaowaunga mkono, wanashindwa kwenye uwanja wa vita.
Aidha, Jenerali Ekenge amesema kilichofanyika hakiwezei kuitwa kitu kingine bali ni uvamizi wa ardhi yake.
Msemaji wa kundi la M 23 Willy Ngoma, amethibitisha kuuteka mji wa Bunagana baada ya kujibu mashambulizi ya wanajeshi wa DRC.
Hatua hii inayumbisha zaidi uhusiano kati ya Kinshasa na Kigali licha ya kuwepo kwa jitihada za kumaliza mvutano huu kwa njia ya kidiplomasia.
M 23 kuudhibiti mji wa Bunagana, umesababisha maelfu ya watu ya watu wanaoishi katika Wilaya ya Rutshkuru kukimbilia katika nchi jirani ya Uganda.