Ethiopia yashtumiwa kwa kuwakamata na kuwahangaisha wanahabari
Wanahabari 13 wamekamatwa nchini Ethiopia, kufuatia mwendelezo wa maafisa wa usalama kuwakamata wanahabari na wanaharakati wa haki za binadamu.
Imechapishwa:
Viongozi katika jimbo la Amhara wanasema watu zaidi ya Elfu nne wamekamatwa katika operesheni ya kuwasaka wahalifu eneo hilo, wakiwemo wanahabari, kwa mujibu wa watetezi wa haki za binadamu, katika hatua ambayo pia imeshtumiwa nje ya nchi hiyo.
Temesgen Desalegn mhariri wa Jarida la Fitih, linaloandikwa kwa lugha ya Amharic ni miongoni mwa wanahabari wanaozuiwa na maafisa wa usalama nchini Ethiopia, na ripoti zinasema alikamatwa na polisi waliokuwa hawajavalia sare.
Aidha, inaelezwa kuwa maafisa wa usalama walifanya msako katika makaazi yake na kuchukua nakala kadhaa za majarida pamoja na Kamera yake.
Mwanahabari mwingine aliyekamatwa ni Yaysewe Shimelis, yeye alichukukuliwa na maafisa wa usalama jijini Addis Ababa baada ya kushtumiwa kuchochea machafuko kupitia mtandao wake wa Youtube.
Marekani na mashirika ya Kimataifa kama Kamati ya kuwatetea wanahabari, na Shirika la Wanahabari wasiokuwa na mipaka, wanataka kuachiwa kwa wanahabari hao na wanataka serikali ya Ethiopia kuacha kuwahangaisha wanababari.