Mauaji yaendelea mashariki mwa DRC mwaka mmoja baada ya hali ya dharura
Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, ni mwaka mmoja kamili tangu kuanzishwa kwa hali ya dharura katika mikoa ya Kivu Kaskazini na Ituri mwaka uliopita, kwa lengo la kuyakabili makundi yenye silaha hasa kundi la waasi la ADF .
Imechapishwa: Imehaririwa:
Hata hivyo, mwaka mmoja baadaye, mauaji yameendelea kushuhudiwa katika majimbo hayo mawili licha ya serikali na jeshi la FARDC kuendelea kuwahakikishia wananchi kuwa, inafanya kile inachoweza kuwalinda.
Kipindi cha huo mwaka mmoja, uhuru wa kujieleza, umezuiwa na jeshi ambalo linaongoza katika majimbo hayo mawili.
Walioathirika zaidi ni Shirika la kupigania haki na demokrasia LUCHA.
"Kila mmoja anayezungumza, anapelekwa gerezani, wakiwemo wanachama wa Lucha waliokuwa wanaandamana, kupinga hali hiyo ya dharura," amesema Steward Mumbere.
Steward Mumbere
Mashirika ya kiraia yanasema, licha ya kuwepo kwa hali hiyo na hata kuja kwa wanajeshi wa Uganda, hakujasaidia kuleta utulivu nchini humo.
“ Viongozi wa kijeshi waliwekwa hapa, tulifikiri kutakuwa na amani ila hilo halijafanyika,” alisema Richard Kirimba mmoja wa viongozi wa mashirika ya kiraia.
Richard Kirimba
Wanasiasa katika mikoa hiyo miwili, wanaona aman inaweza kupatikana tu, iwapo, makamanda wakuu wa jeshi, watahamishwa.
“Watu wengi wameendelea kupoteza maisha, wakuu wa vikosi vya jeshi, wahamishwe,” anasema mbunge Jean Baptiste Kasekwa.
Mbunge Jean Baptiste Kasekwa
Utafiti kutoka shirika linalothmini hai ya usalama la Kivu Barometer Security unasema kwa mwaka mmoja uliopita, katika kipindi hiki cha dharura watu 373 wameuawa baada ya kushambuliwa na makundi yenye siasa.