Jeshi la DRC lawaokoa mateka 150 kutokamikononi mwa ADF
Jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo linasema wanajeshi wake wamefanikiwa kuwaokoa watu zaidi 150 waliokuwa wametekwa na waasi wa ADF, Mashariki mwa nchi hiyo.
Imechapishwa:
Msemaji wa Jeshi kwenye mkoa wa Ituri Jules Ngongo, amesema miongoni mwa watu hao waliokolewa ni wanawake, wazee na watoto.
Aidha amesema hatua hii imewezekana baada ya wanajeshi wa serikali kuwazidi nguvu waasi hao wa ADF katika mapambano yaliyotokea kati ya Julai 18 na 20, katika maeneo ya Boga na Tchabi katika eneo la Irumu.
Jeshi nchini humo linasema raia hao waliotekwa, walikuwa wanatumiwa kama ngao na waasi hao wa ADF wakati wa makabiliano na maafisa wa usalama.
Tangu mwezi Mei mwaka huu, waasi hao wanashtumiwa kuwauwa watu 50 katika maeneo ya Boga na Tchabi, lakini pia kwa kuvamia kambi ya wakimbizi ya Irumu.
Kundi la ADF linasalia kuwa hatari kwa wakaazi wa eneo la Mashariki mwa nchi hiyo.