Benki Kuu nchini DRC yapata Gavana mpya Mwanamke
Malangu Kabedi Mbuyi ameteuliwa kuwa Gavana mpya wa Benki Kuu nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, BCC.
Imechapishwa:
Uteuzi huu unamaanisha kuwa taasisi hiyo nyeti ya kifedha nchini DRC itaongozwa na mwanamke huyo ambaye kabla ya kushika nafasi hiyo, alikuwa mwakilishi wa Shirika la Fedha IMF nchini Burkina Faso.
Wachambuzi wa mambo wanasema, mabadiliko katika Benki hiyo kuu, yalikuwa muhimu kuendana na matakwa ya IMF kabla ya kuipa mkopo wa Dola Bilioni 1.5 nchi hiyo ya Afrika ya Kati.
Bi. Mbuyi anachukua nafasi ya Déogratias Mutombo , ambaye alionekana kuwa mshirika wa karibu wa rais wa zamani Joseph Kabila aliyeshika nafasi hiyo tangu mwaka 2013.
Mabadiliko mengine yaliyofanyika ni kuondoka kwa Albert Yuma, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki hiyo.
Adha, kwa mara ya kwanza, Benki hiyo kuu itakuwa na manaibu wawili wa Magavana kwa mujibu wa mabadiliko yaliyofanyika mwaka 2018 na wawili hao ni washirika wa karibu wa rais Felix Tshisekedi.
Wawili hao ni aliyekuwa Seneta Dieudonné Fikiri na mwanachama wa chama cha siasa UDPS William Pambu.