DRC yatangaza kumalizika kwa mlipuko wa Ebola wa hivi karibuni
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imetangaza kumalizika kwa mlipuko wa ugonjwa wa Ebola ulioripotiwa hivi karibuni na kusababisha vifo vya watu sita na wengine 12 kuambukizwa mkoani Kivu Kaskazini.
Imechapishwa:
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jumatatu hii wizara ya afya imefahamisha kuwa DRC ilifikia uamuzi wa huo miezi mitatu baada ya kupata mafanikio ya chanjo dhidi ugonjwa huo ulioibuka tena huko Kivu Kaskazini mashariki mwa nchi hiyo mwezi february mwaka Huu.
Shirika la Afya Duniani, WHO, limechapisha tangazo hilo kupitia mtandao wake wa kijamii wa Twitter Jumatatu hii.
Mkurugenzi wa WHO kanda ya Afrika Dr. Matshidiso Moeti amepongeza DRC kwa kufanikiwa kutokomeza mlipuko wa hivi karibuni wa ugonjwa wa Ebola uliosababisha vifo vya watu sita.
Waziri Jacques Mbungani amesema Chanjo ya rVSV-ZEBOV (Recombinant vesicular stomatitis virus–Zaire Ebola virus) iliyotengenezwa na maabara ya Amerika Merck Sharpe na Dohme (MSD) ilitumika kuzuia kuenea kwa janga hili la kumi na mbili na kwamba mbali na vifo 6 Jumla ya visa 12 vilirekodiwa, huku akithibitisha kuwa mamia ya watu wamepewa chanjo tangu kuibuka tena kwa janga hilo mnamo Februari 7 katika mkoa wa Kivu Kaskazini, mashariki mwa DRC.