Eritrea yakiri kuwepo kwa wanajeshi wake Tigray, yatangaza kuanza kujiondoa
Eritrea imeliambia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwamba imekubali kuanza kutoa wanajeshi katika jimbo la Tigray nchini Ethiopia, ikikiri hadharani kwa mara ya kwanza kuhusika kwa nchi hiyo katika mzozo huo.
Imechapishwa:
Kukiri huko kwa Eritrea kwa barua kwa wanachama 15 wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa na kurushwa mtandaoni na Wizara ya Habari ya Eritrea, kunakuja siku moja baada ya mkuu wa mashirika ya kutoa msaada, Mark Lowcock kusema hawajaona ushahidi wowote wa kuondolewa kwa wanajeshi wa Eritrea katika jimbo la Tigray.
"Eritrea na Ethiopia wamekubaliana, kuendelea utaratibu wa kuondoa majeshi ya Eritrea na wakati huo huo kutumwa kwa vikosi vya Ethiopia kwenye mpaka wa kimataifa," ameandika Sophia Tesfamariam, Balozi wa Eritrea kwenye Umoja wa Mataifa.
Vikosi vya Eritrea viliwasaidia wanajeshi wa serikali ya shirikisho la Ethiopia kupigana na chama tawala cha zamani huko Tigray katika mzozo ulioanza mnamo mwezi Novemba mwaka jana. Hata hivyo, hadi sasa Eritrea imekataa mara kadhaa uwepo wa vikosi vyake katika eneo hilo lenye milima.