Waasi nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati watangaza kusitisha mapambano
Muungano wa waasi nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, ambao umekuwa ukipambana na serikali jijini Bangui, sasa unasema utasitisha makabiliano yote kuelekea Uchaguzi Mkuu siku ya Jumapili.
Imechapishwa:
Taarifa ya muungano huo wa waaasi, ambao kuanzia Ijumaa iliyopita ulianza vita kwa lengo la kudhibiti jiji kuu la Bangui, imeeleza kuwa imesitisha harakati zake kote nchini kwa muda wa saa 72.
Waasi hao pia wanataka seerikali kuacha mapambano huku wakimtaka rais Faustin Archange Touadera, kuahirisha Uchaguzi wa Jumapili, kwa kile wanachodai kuwa mazingira kwa sasa sio mazuri ya kuendelea na zoezi hilo.
Hata hivyo, msemaji wa serikali Ange-Maxime Kazagui ametupilia mbali tarifa hiyo ambayo amesema kuwa haikuwa imetiwa saini.
Serikali jijini Bangui imeendelea kumshtumu rais wa zamani Francois Bozize kwa kutaka kuchukua madaraka kwa nguvu.
Jumuiya ya Kimataifa inataka utulivu na amani kuelekea Uchaguzi wa Jumapili ambao unaonekana kuwa kipimo kikubwa cha ukomavu wa demokrasia katika taifa hilo ambalo tangu mwaka 2013 imekosa utulivu.