Ripoti: Watu 10,000 wamefariki dunia wakiwa kizuizini tangu mwaka 2011 Nigeria
Katika ripoti ya kurasa 67 iliyotolewa hivi punde, shirika la kimataifa la haki za binadamu la Amnesty International limesikitishwa na hatma ya wazee wanaokabiliwa na vurugu za kundi la Boko Haram na jeshi la Nigeria katika Jimbo la Borno, kaskazini mashariki mwa Nigeria.
Imechapishwa:
Ripoti hii inaelezea jinsi watu hawa wanavyokabiliwa na adhabu mbili kwa mpigo, mateso kutoka kwa kundi hili la kijihadi na ukatili unaotekelezwa na jeshi.
Watu hao hawaonekani kabisa, kulingana na ripoti hii yenye kichwa cha habari "Moyo wangu unavuja damu: maisha ya wazee wanaokabiliwa na mizozo, kuyatoroka makazi yao na kuwekwa kizuizini kaskazini mashariki mwa Nigeria".
Ukatili unaotendewa watu wazee katika Jimbo la Borno ni sawa na "uhalifu wa kivita na hata uhalifu dhidi ya ubinadamu," kulingana na Joanne Mariner, mkurugenzi anayehusika na masuala ya migogoro wa Amnesty International.
Wakati raia wanakimbia vijiji vyao, wakitishiwa na kusonga mbele kwa wanajihadi, wazee mara nyingi hubaki nyumbani, kwa matumaini ya kuendelea kulima mashamba yao kwa minajili ya kupata chakula. Lakini "wengi wao walikufa njaa katika nyumba zao au waliuawa huko," kulingana na ripoti ya Amnesty.