Chad: Kiongozi wa waasi Jamhuri ya Afrika ya Kati Abdoulaye Miskine afikishwa mbele ya jaji
Kiongozi wa waasi Jamhuri ya Afrika ya Kati Abdoulaye Miskine na wahirika wake watatu waliokamatwa mwezi Oktoba mwaka jana nchini Chad wamefikishwa mbele jaji kwa uchunguzi zaidi.
Imechapishwa:
Kiongozi huyo wa waasi, ambaye serikali ya Bangui inataka asafirishwe nchini Jahuri ya Afrika ya Kati, ameanzisha mchakato wa kisheria ambao unaweza kuchukuwa muda mrefu nchini Chad.
Siku ya Ijumaa ya wiki iliyopita wakati walikabidhiwa mahakama kutoka mikononi mwa idara ya ujasusi tangu mwezi Oktoba, Abdoulaye Miskine na wenzake watatu hawakuweza kukutana na jaji ili kuamua juu ya hatma yao, kwa mujibu wa mwandishi wetu huko Ndjamena, Madjiasra Nako.
Hata hivyo Jumatatu Juni 1, mkuu wa majaji wanahusika na uchunguzi alipata taarifa kuhusu kesi yao na kuamua kuwatuma jela.
"jaji amewafahamisha makosa mawili yanayowakabili, ambayo ni kuunda na kusimamia kundi la uasi pamoja na ubakaji, na kuamua kuwaweka chini ya waranti wa kukamatwa wakiwa katika gereza la N'djamena," Mognan Kembetiade, mmoja wa mawakili wao amesema.
Kulingana na vyanzo vya mahakama, Chad, ambayo imeendelea kupinga ombi la kusafirishwa kwa watuhumiwa hao nchjini Jamhuri ya Afrika ya Kati, inataka kuwafungulia mashitaka kuhusu uhalifu uliotendewa raia wake wakati wa machafuko nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, uhalifu ambao Chad inasema ulitekelezwa na wapiganaji wa Abdoulaye Miskine na wenzake.
Wakati huo huo, Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai na vyombo vya sheria nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, ambavyo vinawahaitaji watu hao, vitalazimika kusubiri.