Coronavirus: Nchi kadhaa za Afrika kuanza kutumia dawa kutoka Madagascar
Wakati wanasayansi duniani wakihangaika kupata chanjo na tiba ya virusi vya Corona, hivi karibuni rais wa Madagascar Andry Rajoelina alizindua dawa ya mitishamba ''inayotibu'' ugonjwa wa Covid-19.
Imechapishwa:
Kwa wiki mbili sasa, rais Andry Rajoelina amekuwa akifanya mazungumzo na viongozi wenzake wa nchi za Afrika. Ndege ya nchi ya Equatorial Guinea iliwasili Jumatano alasiri jijini Antananarivo ili kuweza kubeba tani 1.5 za dawa hiyo.
Wakati huo huo ndege nyingine kutoka Guinea-Bissau inatarajiwa kutua leo Alhamisi kwenye uwanja wa Antananarivo, Madagascar.
Hata hivyo Shirika la Afya Duniani (WHO) linasema kuwa hakuna ushahidi wa tiba ya Covid-19 baada ya Bwana Rajoelina kutangaza dawa yake.
Nayo Taasisi ya taifa ya tiba nchini Madagascar (Anamem) pia imeonyesha wasiwasi wake juu ya ufanisi wa dawa hiyo inayoelezewa na rais Andry Rajoelina kama yenye uwezo wa kuzuwia na kupona corona.
Wakati wa mazungumzo yake na Andry Rajoelina, Umaro Sissoco Embalo, rais wa Guinea-Bissau alisema kwamba "anaweza kuchukuwa dawa hiyo kutoka Madagascar na kuisambaza kwa wanachama wa Jumuiya ya Kiuchumi ya nchi za Magharbi mwa Afrika, ECOWAS, yaani nchi 15.
Hii tayari imeshakubaliwa na Senegal na Togo hasa ", amesema mkurugenzi wa afisi ya rais wa Madagascar, Lova Hasinirina Ranoromaro.