Minembwe yaendelea kukumbwa na jinamzi la mauaji
Kufuatia mapigano ya kikabila yanayoendelea kushuhudiwa katika eneo la Minembwe na maeneo mengine ya Bonde la Ruzizi na Fizi, tume ya Umoja Mataifa nchini DRC, MONUSCO, imependekeza kuanzishwa kwa operesheni ya kuwapokonya silaha wapiganaji wanaowakilisha makabila yao katika eneo hilo.
Imechapishwa:
Kauli hii imetolewa wakati huu hali ya usalama imeendelea kuzorota katika eneo hilo ambako mamia kwa maelfu ya wakaazi wamelazimika kuyatoroka makazi yao kufuatia mapigano kati ya makundi ya mai mai na wapiganaji wengine wenye silaha katika eneo la Minembwe.
Katika mji wa Minembwe, hasa katika maeneo ya milimani, jeshi la DRC (FARDC) na kikosi cha Umoja wa Mataifa nchini humo, MONUSCO wameimarisha ngome zao lakini mauaji hayo yanaendelea.
Katika maeneo mbalimbali ya wilaya ya Minembwe, nyumba zimekuwa zikiteketea kwa moto. Mifugo, hasa Ng'ombe wametoweka. Wakaazi wengi walitoroka vijiji vyao na kukimbilia katikati mwa mji. Watu kutoka jamii ya Wanyamulenge ndio pekee wamesalia vijijini lakini hivi karibuni Eli Ntambara, mwakilishi wa jamii hiyo, alisema hali hiyo isiambatanishwi mgogoro wa kikabila.
Tangu mwezi Septemba mwaka huu, watu kutoka jamii zingine katika eneo la Minembwe walitoroka makaazi yao. Kuna wafanyabiashara wachache tu kutoka jamii ya Washi ambao wamebaki, lakini pia mwakilishi wa jamii ya Wafuliro.