Mdororo wa usalama na vitisho vyaripotiwa DRC
Wanahabri wawili wa DRC wamelazimika kutoroka mjini Bukavu baada ya kupeperusha kipindi maalum cha Televesheni kuhusu namna raia wanavyoteswa na kufukuzwa kwa ardhi inayoaminiwa kuwa ni ya rais Joseph Kabila.
Imechapishwa:
Mashirika ya kutetea haki za binadamu yameitaka serikali kuwahakikishia usalama wanahabari hao.
Shirika la Kimataifa linalowatetea wanahabari RSF limesema, wanabahari nchini DRC wanaotoa ripoti kama hizo wamendelea kutishwa.
Hayo yanajiri wakati ambapo kwa mujibu wa vyanzo vya usalama watu 15 wameuawa kwa kipindi cha siku tano, wakati wa makabiliano kati ya makundi ya waasi Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Kiongozi wa serikali katika Wilaya ya Masisi, Cosmas, Kangakolo amesema mapigano hayo yamekuwa yakiendelea katika maeneo ya Kamiro,Lukweti na Nyabiondo.
Hata hivyo, jeshi linasema limefanikiwa kuwashinda waasi hao.
Mashariki mwa DRC inaaminika kuwa kuna makundi ya waasi zaidi ya 70 ambayo yanaendelea kusumbua raia.
Wakati huo huo Tume ya Umoja wa Mataifa MONUSCO inayashtumu makundi ya waasi kuendesha vitendo vya ukiukwaji wa haki za binaadam zaidi ya 1000 katika mkoa wa Kivu Kaskazini ikiwa ni pamoja na kuwabaka wanawake zaidi ya 200 ,tangu kuanza kwa mwaka huu.