Watu 15 wauawa katika mapigano kati ya jeshi na waasi Kasai, DRC
Watu 15 wameuawa katika jimbo la Kasai nchini DRC baada ya mapigano kati ya waasi wa Kamwina Nsapu na jeshi la serikali. Wadadisi wanasema hali ya Usalama nchini DRC inaendelea kutisha.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Serikali ya DRC inasema waasi hao waliwashambulia wanajeshi katika eneo la Lombelu, na kusababisha majibizano makali ya silaha.
Ripoti zinasema kuwa, nusu ya waliopoteza maisha ni raia wa kawaida waliojikuta katika makabiliano hayo.
Zaidi ya watu 3,000 wamepoteza maisha katika jimbo la Kasai kwa mujibu wa takwimu za Kanisa Katoliki tangu mwaka 2006, wakati kiongozi wa waasi hao alipouliwa na serikali.
Hayo yanajiri wakati ambapo zaidi ya watu 22 waliuawa katika machafuko ya kikabila yaliyotokea mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo siku tatau zilizopita, kwa mujibu wa shirika la habari la Reuters, likinukuu chanzo rasmi.
Wanamgambo wa Nyatura, kundi linaloundwa na wanamgambo wengi kutoka jamii ya Wahutu, walishambulia waasi wa kundi la Mai-Mai Yakutumba, wa kikabila la Nande, katika kijiji cha Kalusi siku ya Jumapili na Bwalanda siku ya Jumatatu.
Vurugu za kikabila na mashambulizi ya jeshi la serikali dhidi ya waasi vimesababisha vifo vya mamia ya watu katika miezi ya hivi karibuni nchini DRC na maelfu ya watu kulazimika kuyahama makazi yao.