Nigeria: Wanafunzi 110 hawajulikani walipo
Wiki moja baada ya shambulio dhidi ya shule huko Dapchi kaskazini mashariki mwa Nigeria, na baada ya siku sita za mkanganyiko, hatimnaye serikali imetangaza idadi kamili ya wasichana waliotoweka na hawajapatikana mpaka sasa.
Imechapishwa:
Serikali ya Nigeria imethibitisha kwamba wanafunzi wasichana 110 walitoweka baada ya shambulio dhidi ya shule yao. Shambulio lililoendeshwa na wapiganaji wa kundi la Boko Haram.
"Wanafunzi mia moja na kumi wametoweka na hawajapatikana mpaka sasa, " Waziri wa Habari, Lai Mohammed, alitangaza siku ya Jumapili usiku, Februari 25.
Wakati huo huo mamlaka nchini Nigeria imesema imeongeza nguvu ya ndege za kivita ili kuhakikisha imewapata wanafunzi wasichana waliotekwa Kaskazini Mashariki mwa nchi hiyo.
Mapema wiki hii iliyopita serikali ya kijiji hicho ilililaumu jeshi kwa kushindwa kuchukua hatua hata baada ya kupewa taarifa.
Rais Muhammadu Buhari ameelezea tukio hilo kama janga la taifa.
Wiki moja baada ya tukio hilo, hakuna kundi hata moja ambalo limedai kuhusika na shambulio hilo. Hata hivyo kundi la Boko Haram limeendelea kunyooshewa kidolea cha lawama kuwa ndio limehusika na shambulio hilo. Lakini kwa baadhi ya waangalizi wanasema inawezekana kuwa shambulio hilo likawa limetekelezwa na kundi la wahalifu linalotaka fidia.