Boko Haram: tutawaachia wasichana kwa kubadilishana na wafungwa
Kiongozi wa kundi la Boko Haram Abubakar Shekau ameweka wazi mkanda wa video unaowaonyesha wasichana zaidi ya mia moja ambao wanashukiwa kuwa wanafunzi waliotekwa hivi karibuni na kundi hilo kaskazini mwa Nigeria na kuthibitisha kwa wote wamesilimu na kuwa waislam.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Katika mkanda huo wenye dakika 27, Abubakar Shekau ameomba wafungwa wote kutoka kundi la Boko Haram waachiwe huru kabla ya kuwaacha wasichana hao ambao ametishia kuwaoza kwa bei kubwa, huku wasichana hao wakionekana wote wamevaa hijabu na kuendelea kusoma Coran katika hali tulivu.
Jumla wasichana 276 ndio wanaoshikiliwa na kundi hilo tangu April 14 huko Chibok katika Jimbo la Borno kaskazini mashariki mwa Nigeria ambako kunaeshi wa kristo wengi. Polisi inasema wasichana 223 hawajulikani walipo.
Mkanda huo wa video unawaonyesha takriban wasichana 130 waliovalia hijabu nyeusi na yenye rangi ya kijivu, wakifunika nyuso zao wakikaa chini eneo linalo fanana na msituni huku wakisoma Coran. Hii hapa video iliyowekwa wazi na kundi la Boko Haram jumatatu hii.
Hadi sasa inekuwa vigumu kujuwa ni wapi walipo wasichana hao, licha ya jumuiya ya kimataifa kutuma wataalam wa ujasusi kwa ajili ya kuwasaka walipo.
Haijulikani wapi ulitengenezwa mkanda huo wa video, kwani ulitengenezwa kwa ustadi ikilinganishwa na mikanda mingine ya video inayotengezwa na wanamgambo wa makundi ya kiislamu. Katika mkanda huo ameonekana mtu akivalia mavazi ya kijeshi huku akishikilia Kamera mkononi.
Ameonekana katika mkanda huo, kiongozi wa kundi la Boko Haram, Abubakar Shekau, akivalia mavazi ya kijeshi, akibebelea bunduki aina ya kalachnikov begani, huku akidhihirisha furaha yake.
Akiongea kwa lugha ya kiarabu na kihausa, lugha inayozungumzwa zaidi kaskazini mwa Nigeria, Abubakar Shekau, amekiri kwa mara nyingine tena kuwateka wasichana hao.
Baada ya Marekani,Uingereza na Ufaransa ambayo imewatuma hivi karibuni wataalamu nchini Nigeria ili kusaidia kikosi cha usalama kutafuta wasichana hao waliotekwa na kundi la Boko Haramu.
Hapo jana Israeli imesema kama iko tayari kushirikiana na mataifa mengine kwa kuwatafuta wasichana hao.
Hayo yakijiri, rais wa Ufaransa Francois Hollande, jana amependekeza kufanyika kikao mjini Paris siku ya jumamosi kuhusu usalama nchini Nigeria, kikao ambacho kitaishirikisha Nigeria na mataifa manne jirani, ambayo ni Chad, Cameroon, Niger na Benin.