Mwanamke anayedaikuwa alibakwa na wanajeshi wa AMISOM aeleza madhila yalivyomkuta
Mwanamke mmoja huko Somalia anayedai kuwa alitekwa nyara, kuchomwa sindano ya dawa na kubakwa na kundi la Wanajeshi wa Umoja wa Afrika walio katika Operesheni nchini Somalia, AMISOM ameeleza namna alivyokutwa na madhila hayo.
Imechapishwa:
Amesema kuwa wanajeshi walimbaka na alipojaribu kujitetea aliambulia kipigo hali iliyomfanya kupoteza fahamu, Mwanamama ameeleza katika mahojiano yake na kituo cha televisheni ya nchini Somalia akielezea mkasa uliompata mapema mwezi huu.
Awali Kikosi cha AMISOM kilikiri kimepokea shutma hizo dhidi ya Wanajeshi wake. Kauli ya AMISOM imesema kuwa jeshi lake na lile la Somalia limeandaa kikosi ambacho kitafanya uchunguzi na baadae hatua stahiki zitachukuliwa baada ya kubainika ukweli juu ya shutuma hizo.
Jeshi la AMISOM, lina Wanajeshi 17,700 ambao walipatiwa mamlaka ya kuisaidia Serikali ya Somalia kupambana na Wanamgambo wenye uhusiano na Kundi la Al Qaeda, Al Shabaab.
Ikiwa itathibitika kuwa kweli Wanajeshi wa Vikosi hivyo wamejihusisha na vitendo vya ubakaji itaathiri heshima ya Vikosi vya Umoja wa Afrika iliyojiwekea mbele ya uso wa
JumuiYa ya kimataifa. Jeshi la Somalia awali liliwahi kushutumiwa na makundi ya kutetea haki za binaadam kuwa Wanajeshi wake wamekuwa wakijihusisha na vitendo vya unyanyasaji dhidi ya Wanawake vikiwemo vitendo vya ubakaji.
Jeshi hilo limesema kuwa linafanya uchunguzi kubaini waliohusika na katika visa hivyo vya ubakaji na kuwa hatua zitachukuliwa ikiwa itathibitika kuwa walihusika.