Maandamano ya kuunga mkono na kupinga utawala wa Morsi yaendelea nchini Misri
Mamia kwa maelfu ya raia wa Misri wameendelea kuandamana wakishinikiza kujiuzulu kwa Rais Mohamed Morsi aliyekaa madarakani kwa mwaka mmoja toka achaguliwe katika uchaguzi wa kwanza wa kidemokrasia.
Imechapishwa:
Watu zaidi ya watano wamekufa na mamia kujeruhiwa katika ghasia za jana Jumapili zilizoanzia katika viwanja vya Tahrir mjini Cairo na kuenea katika miji mbalimbali nchini humo.
Muungano wa wapinzani umeendelea kutoa wito kwa waandamanaji kusalia mitaani mpaka kiongozi huyo atakapoachia ngazi kwani amekiuka misingi ya utawala wa kidemokrasia kama walivyotarajia baada ya mapinduzi ya mwaka 2011.
Wafuasi wa chama cha Muslim Brotherhood nao wamejikusanya katika maeneo mbalimbali wakiendesha maandamano ya kumuunga mkono kiongozi huyo ambaye kwa sasa amesema anataka kufanya majadiliano na wapinzani ili kutafuta suluhu ya mgogoro huo na kuepusha umwagaji damu.