Washukiwa wa mauaji ya Kiongozi wa upinzani nchini Tunisia wakamatwa
Mshukiwa anayeshutumiwa kutekeleza mauaji dhidi ya kiongozi wa upinzani nchini Tunisia Chokri Belaid aliyekuwa mkosoaji mkubwa wa Chama Tawala chenye mrengo wa kiislamu, amekamatwa na Polisi.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Polisi wamesema kuwa wamemkamata mshukiwa huyo kufuatia ushahidi wa Mwanamke mmoja aliyedai kuwa alishuhudia mauaji hayo hali iliyofanya Polisi kutoa ulinzi kwa mwanamke huyo.
Familia ya Marehemu Belaid imeshutumu chama tawala cha Ennahda kwa kile walichodai kuwa Chama hicho kimehusika na mauaji hayo, madai ambayo chama hicho kimepinga.
Mauaji dhidi ya Belaid yalisababisha kuzuka kwa mtafaruku na maandamano makubwa kukemea mauaji hayo.
Kutokana na hali hiyo, Waziri Mkuu wa Tunisia, Hamadi Jebali alipendekeza kuundwa kwa Serikali itakayokuwa na Viongozi ambao ni Wataalam ili kumaliza mzozo nchini Tunisia, hatua iliyopingwa na baadhi ya Wafuasi wa Ennahda.