Watalii wawili raia wa Ujerumani waliokuwa wametekwa nchini Ethiopia waachiwa huru
Waasi wa nchini Ethiopia wametangaza kuwaachilia huru raia wawili wa Ujerumani ambao ilikuwa inawashikiliwa tokea tarehe 18 ya mwezi January baada ya kutokea mapigano kati yake na polisi kwenye eneo la jangwa la Afar.
Imechapishwa:
Kwenye utekaji nyara huo watu watano walipoteza maisha ambapo waasi hao walifanikiwa kuwateka raia hao wawili wa Ujerumani na kutishia kuwaua endapo serikali ya Ethiopia haitawaachia baadhi ya wafuasi wake.
Kwa mujibu wa taarifa ambayo imetolewa na kundi la The Afar Revolutionary Democratic Unity Front ARDUF, imesema kuwa imewaachilia huru raia hao wawili na kuwakabidhi kwa maofisa wa ubalozi wa Ujerumani
Taarifa ya kundi hilo imeongeza kuwa linaomba radhi kutokana na vifo vya raia wengine waliopoteza maisha kwenye shambulio hilo na kuilaumu serikali ya Ethiopia kwa kuendelea kuwaingilia kwenye maeneo yao wanayoyashikilia.
Viongozi wa serikali ya ethiopia hawakupatikana mara moja kuzungumzia tukio hilo.
Waasi hao wa ARDUF wamekuwa wakiendesha operesheni zao kwenye eneo la jangwa la Erta ale na mara kadhaa limekuwa likiwateka nyara watalii wanaofika kutembelea maeneo hayo.