Mpinzani mkuu nchini Liberia atangaza kususia duru ya pili ya uchaguzi wiki ijayo
Wiston Tubman Mgombea wa urais wa chama kikuu cha upinzani nchini Liberia cha CDC, ametangaza kujitoa kwenye kinyanganyiro hicho cha uchaguzi wa marudio unaofanyika Novemba nane mwaka huu. Halii hii inaashiria ushindi wa chama tawala, lakini huenda ikaondoa uhalali wa mchakato wa uchaguzi nchini humo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Tubman amesema anagomea uchaguzi huo wa Jumanne dhidi ya Rais Ellen Johnson-Sirleaf, kwa sababu haamini kuwa utakuwa wa haki. Sirleaf anatarajiwa kushinda uchaguzi huo wa marudio, baada ya kupata asilimia 44 katika uchaguzi wa mwanzo, mwezi uliopita.
Uchaguzi huu wa rais unachukuliwa kama kipimo kwa demokrasia changa ya Liberia, ambao unafanyika miaka minane baada ya kumalizika vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyochukuwa miaka 14 na kugharimu maisha ya watu laki mbili na nusu.
Rais Ellen Johnson-Sirleaf wa Liberia amewataka wapiga kura nchini mwake waupuuze wito wa mpinzani wake wa kuisusia duru ya pili ya uchaguzi wa rais wiki ijayo. Rais Sirleaf ameuita wito wa Winston Tubman kuwa ni kinyume na sheria na kwamba umelengwa kuwatisha wananchi wa Liberia.