Mkutano wa ANC kujadili hatima ya Zuma waahirishwa
Mkutano wa chama tawala nchini Afrika Kusini, ANC, kuhusu kujadili hatima ya rais wa nchi hiyo Jacob Zuma, uliokua ulipangwa kufanyika jana Jumanne uliahirishwa.
Imechapishwa:
Mkutano wa jana Jumanne wa chama cha ANC ulisogezwa mbele hadi juma lijalo kupisha mazungumzo zaidi kufanyika wakati huu shinikizo zaidi likiongezeka kwa rais Zuma kuondoka madarakani kutokana na kashfa za rushwa zinazomkabili.
Bunge la nchi hiyo likitangaza kuahirishwa hotuba aliyokuwa aitoe bungeni hapo kesho Alhamisi hali inayozidisha sintofahamu zaidi kuhusu mustakabali wake.
Hata hivyo baadhi ya mitandao nchini humo imekaririwa ikisema kuwa rais Zuma anajiandaa kuachia madaraka iwapo makubaliano katiika mambo kadhaa yatafikiwa.
Jana Jumanne wakuu wa chama tawala cha ANC wamesema walikuwa na mazungumzo yenye tija kuhusu mustakabali wa rais Zuma na kwamba wamefikia hatua nzuri, matamshi yaliyotolewa saa chache kabla ya kutangazwa kufutwa kwa hotuba yake.
Upinzani unashinikiza Zuma kupigiwa kura ya kutokuwa na imani naye, huku kikao cha kamati kuu kikidaiwa kuwa na nguvu ya kuweza kumuondoa Zuma madarakani hata bila hiari yake.
Mkutano wa kamati kuu ya chama hicho NEC unatarajiwa kufanyika Februari 17 na 18 kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na kiongozi wa chama hicho cha ANC Cyril Ramaphosa.