Trump kutoanzisha uchunguzi kuhusu barua pepe za Clinton
Rais mteule wa Marekani Donald Trump amesema hatoanzisha uchunguzi mwengine kuhusu barua pepe za Hillary Clinton ili kumsaidia ''kuondokana na tatizo hilo''. Donald Trump alitishia kumfunga jela Bi Clinton na katika mikutano yake wafuasi wake walimuunga mkono kwa kusema 'mfunge jela'.
Imechapishwa:
Mshauri mkuu wa Trump, Kellyanne Conway amesema kuwa Trump hatotekeleza ahadi yake ya kumteua mwendesha mashtaka ili kumchunguza aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Hillary Clinton.
Mkurugenzi wa shirika la kijasusi nchini Marekani James Comey alimuondolea makosa Bi Clinton.
Bi Conway alimwambia mtangazaji wa kipindi cha alfajiri cha MSNBC Joe Scarborough: "Nadhani wakati rais mteule ambaye pia ni kiongozi wa chama chenu sasa, anasema kabla hajaapishwa hapendelei kumfungulia mashtaka Hillary Clinton, ni ujumbe mzito sana kwa wanachama wa Republican."
''Na nadhani Hillary Clinton anafaa kujua kwamba raia wengi wa Marekani hawana imani naye, lakini Donald Trump anaweza kumsaidia kuendelea na maisha yake akiwa huru, basi pengine kwamba hilo ni jambo zuri kwa muhusoka mwenyewe na familia yake pia ," amesema Bi Conway.