Pata taarifa kuu

Alliance na azma ya kuwa kituo kikubwa cha uandalizi wa wanasoka duniani

Kituo cha Michezo Alliance sio jina ggeni masikioni mwa mashabiki wa soka Tanzania na pengine eneo zima la Afrika mashariki.Ni hapa ambapo mwaka 2011 kulindikwa historia ya kuzinduliwa kwa shule ya msingi na baadaye sekondari kulikofanywa na mkurugenzi mwanzilishi wa shule hizo James Bwire.

Makao makuu ya kituo cha Alliance kilichopo Mwanza, Kaskazini Magharibi mwa Tanzania
Makao makuu ya kituo cha Alliance kilichopo Mwanza, Kaskazini Magharibi mwa Tanzania RFI Kiswahili/Fredrick Nwaka
Matangazo ya kibiashara

Septemba 19, 2019 nikiwa katika ziara ya kikazi mkoani Mwanza, Kaskazini magharibi mwa Tanzania, nilifika kituoni hapo, umbali wa karibu kilomita moja na nusu kutoka kituo cha mabasi cha Buzuruga.

Ni eneo kubwa lenye majengo ya shule, maeneo ya ofisi za kituo cha michezo huku eneo lingine lililopo mbali likiwa na viwanja pamoja na hosteli za wachezaji.
"Zaidi ya milioni 500 zilitumika kuanzisha kituo hiki miaka minane iliyopita,"anasema Yusuph Budodi, Afisa anayeshughulikia mashindano kituoni hapo.

Mbali na kusomea taaluma ya michezo katika chuo cha michezo cha Butimba kilichopo Mwanza, Mkurugenzi wa kituo hicho James Bwire kuhudhuria mafunzo ya kuda mfupi katika nchi za Kenya, Uganda na hata Rwanda.

Macho yangu kwa harakaharaka yananipeleka kuangalia eneo la ofisi ambapo Budodi ananiongoza kwa ajili ya kufanya mahojiano naye.

"Tupo hapa, tumeshiriki mashindano mbalimbali ya vijana katika nchi za Afrika mashariki na kati na vikombe tulivyotwaa ni hivi,"
Ni ofisi ndogo kiasi lakini ina kabati lililosheheni vikombe mbalimbali. Kwa hakika inavutia kuona namna kituo hiki kilivyojipanga.

Mafanikio

Kuhusu mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka minane ya uhai wa kituo hicho Budodi ansema si makubwa kwakuwa mpira unahitaji uvumilivu.
"Tumeongeza idadi ya vijana kutoka 12 tulioanza nao 2011 na sasa tuna idadi ya karibu vijana miamoja na dhamira ni kuwa kitovu cha uzalishaji wa wanasoka hapa Tanzania,"

Msimu huu klabu hiyo ilipata mafanikio nje ya uwanja baada ya kumuuza mshambuliaji wake Mapinduzi Balama kwa klabu kubwa ya soka Tanzania ya Yanga.

"Ni mafanikio ya kwanza nje ya uwanja, tumepata fedha ambazo zinasaidia kuendeleza mambo mbalimbali kituoani hapa, lakini mpira unahitaji uvumilivu.
Pia kituo hicho kimeshiriki mashindano ya vijana katika nchi za Afrika mashariki na kati ambapo kilifanikiwa kufanya vyema.

Pia timu za taifa za Tanzani za vijana zimenufaika na uwekezaji wa Alliance. Mathalani wachezaji Ally Msengi, Andrew Mwenda na Ally Ng'anzi wamezitumikia timu za taifa za vijana huku Ng'anzi akianza kujumuishwa katika kikosi cha timu ya Taifa ya Tanzania "Taifa Stars"

Kwa sasa Ng'anzi anacheza soka la kulipwa nchini Marekani.
Kituo hiki pia kimefanikiwa kuanzisha timu ya wanawake ambayo sasa inacheza ligi kuu ya wanawake ya Tanzania Bara.

"Hii timu ya wanawake ilikuwa ya riadha lakini tulipata changamoto kutoka kwa viongozi wa mpira na mwishowe tukaamua kuibadili kuwa ya soka la wanawake. Tulianza daraja la chini na sasa tupo ligi kuu.

Yusuph Budodi, Mwenyekiti wa kamati ya mashindano Alliance akionyesha vikombe ambavyo kituo hicho kimewahi kushinda.
Yusuph Budodi, Mwenyekiti wa kamati ya mashindano Alliance akionyesha vikombe ambavyo kituo hicho kimewahi kushinda. Fredrick Nwaka

Changamoto kadhaa

Changamoto si haba kama ilivyo kwa vituo mbalimbali vya kukuza soka barani Afrika.

Budodi anataja mawakala feki wa wachezaji ambao huwarubuni baadhi ya wachezaji kutoka kituo hiki.

"Hili ni tatizo kubwa, tunaandaa wachezaji tangu wadogo lakini wanakuja mawakala na kuwarubuni na kuwachukua, mfano kwa mchezaji Israel Mwendwa"anasema Budodi.

Changamoto nyingine ni kwamba kituo baadhi ya wachezaji vijana kushindwa kusimamia misingi ya makubaliano baina ya kituo na wazazi.

"Tunapomchukua mchezaji tunaingia mkataba na familia na mchezaji atasomeshwa na kucheza mpira lakini kuna wengine wanakuja hapa hawataki shule bali wanacheza mpira, hii ni changamoto kwa kuwa mwishowe wachezaji hawa tunawapoteza.

Changamoto nyingine ni uendeshaji wa kituo ambapo Budodi anasema gharama zinaongezeaka siku hadi siku.

Baada ya mahojiano napata fursa ya kutembelea maeneo ya viwanja na hosteli za wachezaji na akilini mwangu inanijia picha ya namna suala la uwekezaji katika soka si lelemama.

Kwa hakika nusu saa niliyokaa katika kituo cha Alliance nilijifunza mengi kuhusu uwekezaji wa soka la vijana.

 

Wito
Budodi anatoa wito kwa mamlaka za soka Tanzania kuthamini vituo vinavyowekeza katika soka la vijana.

"TFF isaidia vituo kama sisi, hata kwa kutupatia mipira tu lakini pia serikali iongeze fedha kwa kwenye ichezo bado kuna mambo mengi ya kufanya. Ninaamini gtukiwa na vituo kumi soka la Tanzania litapiga hatua,"anafafanua.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.