Kombe la Dunia 2018: Croatia yasherehekea ushindi wake Zagreb
Croatia imeendelea kusheherekea ushindi wake dhidi ya Uingereza Jumatano wiki hii, baada ya vijana hao wa Luka Modric kuwaadhabu vijana wa Gareth Southgate baada ya muda wa ziada. Timu ya Luka Modric ilishinda 2-1 dhidi ya vijana wa Gareth Southgate.
Imechapishwa:
Mashabiki wa Croatia walisherehekea usiku kucha baada ya taifa lao kuwaondoa England kutoka kwa michuano ya Kombe la Dunia Urusi na kufuzu kwa fainali kwa mara yao ya kwanza kabisa. WAkati huo huo Uingereza imeendelea kuomboleza kipigo cha mabao mawili kwa bao lao la kufutia machozi.
Uingereza ndio ilianza kuliona lango la Croatia katika dakika ya tano ya mchezo, bao ambalo lilifungwa na
Kieran Trippier. Croatia ilisawazisha katika dakika ya 68 kupitia Ivan Perisic. Bao la pili ambalo ni la ushindi lilifungwa na Mario Mandzukic katika dakika ya 109.
Licha ya ushindi huo, mashabiki wa Croatia wana wasiwasi na timu ya taifa ya Ufaransa, Les Bleu, ambapo baadhi wameanza kukata tamaa.
"Jihadharini na timu ya taifa ya Ufaransa itawafunga. Nimetaka tu kuwatahadharisha. Sisi Wacroatia kwa sasa tuko juu! "amesema mwanamke mmoja wa Croatia.
Croatia watakutana na Ufaransa katika uwanja wa Luzhniki mjini Moscow Jumapili kwa fainali saa tatu usiku saa za Afrika Mashariki.
Nayo Uingereza itamenyana na Ubelgiji mechi ya kuamua atakayemaliza nafasi ya tatu. Mechi hiyo itachezewa katika uwanja wa St Petersburg.