Mashindano ya riadha ya dunia kwa vijana yaanza nchini Kenya
Mashindano ya riadha ya dunia kwa vijana wasiozidi miaka 18 yameanza rasmi jijini Nairobi chini Kenya.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kenya imekuwa nchi ya pili barani Afrika kuandaa mashindano haya makubwa baada ya Morocco kufanya hivyo mwaka 2005.
Haya ni makala ya 10 na ya mwisho kwa mujibu wa Chama cha riadha duniani IAAF, ambacho kimesema mashindano haya ya kila baada ya miaka miwili, sasa yatakuwa yanaandaliwa katika mabara mbalimbali.
Makala ya kwanza ya mashindano haya yalifanyika mwaka 1999 jijini Bydgoszcz nchini Poland .
Marekani inashikilia rekodi ya kushika nafasi ya kwanza katika mashindano haya mara sita, kwa kunyakua medali nyingi, mwaka 2001, 2003, 2005, 2007, 2011 na 2015.
Kenya inafuata kwa kushinda mara mbili mwaka 1999 nchini Poland na 2009 , huku Jamaica wakishinda mara moja mwaka 2013 wakati yalipoandaliwa mjini Donestsk nchini Ukraine.
Mashindano haya ya siku tano, yatakayomalizika siku ya Jumapili, yanafanyika katika uwanja wa Kimataifa wa Moi Kasarani.
Wanariadha zaidi ya 1,400 kutoka mataifa 130 wanashiriki katikamashindano haya.
Maelfu ya maafisa wa usalama wanapiga doria nje ya uwanja wa Kasarani na maeneo jirani kuhakikisha kuwa kuna usalama wa kutosha.