Cristiano kuhojiwa kuhusu ukwepaji wa kodi huku Mourinho akitajwa
Mshambuliaji wa klabu ya soka ya Real Madrid Cristiano Ronaldo, ametakiwa kufika Mahakamani tarehe 31 mwezi Julai mwaka huu, kujibu mashtaka ya kukwepa kulipa kodi.
Imechapishwa:
Serikali ya Uhispania inamtuhumu raia huyo wa Ureno kukwepa kulipa kodi inayokadiriwa kuwa Dola Milioni 16.5.
Mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 32, amekanusha madai hayo kuwa hajalipa kodi hiyo kama inavyodaiwa kati ya mwaka 2011 na 2014.
Madai hayo yamemkerea mchezaji huyo na hata kutishia kuachana na klabu hiyo.
Wakati uo huo, kocha wa klabu ya Manchester United Jose Mourinho pia ametuhumiwa kukwepa kulipa kodi inayokadiriwa kuwa Dola 3.7 alipokuwa kocha wa Real Madrid.
Mourinho anatuhumiwa kukwepa ulipaji kodi kati ya mwaka 2010 na 2013.