PSG: Polisi wanachunguza tukio la wachezaji kushambuliwa na mashabiki wenye hasira
Klabu ya Paris St-Germain ya Ufaransa, imesema uchunguzi wa polisi unaendelea baada ya mashabiki wenye hasira wa timu hiyo kuwakabili wachezaji wa timu hiyo wakati walipowasili kwenye uwanja wa ndege wa Bourget, ambapo timu hiyo ilitolewa na FC Barcelona.
Imechapishwa:
Mabingwa hao wa Ufaransa walisafiri kurejea nyumbani wakitokea mjini Catalonia, ambako walishuhudia ikipata kipigo cha mabao 6-1, huku Barcelona ikipindua matokeo ya awali ya kufungwa mabao 4-0.
Mashabiki hao wa soka waliwatukana wachezaji na kuharibu magari yao katika hali ambayo inaelezwa ilikuwa mbaya zaidi na ya kutisha, klabu hiyo imesema.
Klabu hiyo imeongeza kuwa katika vurugu hizo mtu mmoja aligongwa na gari.
Taarifa ya klabu imesema imesomeka kuwa "Wachezaji walifuatwa na kutishiwa na baadhi ya mashabiki kwenye uwanja wa ndege wa Bourget, licha ya klabu na polisi kuimarisha usalama.
"Watu hawa walikuwa wanatoa maneno makali kwa wachezaji kabla ya kuanza kushambulia magari yao, ambapo magari kadhaa yaliharibiwa vibaya."
"Mtu mmoja aligongwa na gari wakati alipokuwa akijaribu kuukimbia umati wa watu ambao ni dhahiri ulikuwa ukiwatishia wachezaji na familia zao. Uchunguzi wa polisi unaendelea kubaini hasa nini kilitokea."
"Klabu na wale wote waliokuwepo wamewaeleza wapepelezi kuhusu utayari wao kushirikiana na vyombo husika ili kufikia sababu na chanzo cha vurugu zenyewe."