Arsenal yalazimisha sare ya bao 1-1 dhidi ya Manchester United
Klabu ya soka ya Manchester United imetoka sare ya bao 1-1 na Arsenal katika mchuano muhimu wa ligi kuu ya soka nchini Uingereza.
Imechapishwa:
United wakiwa nyumbani katika uwanja wake wa Old Trafford, ilikuwa ya kwanza kupata bao kupitia Juan Mata katika dakika ya 69 ya mchuano huo.
Hata hivyo, dakika ya 89, dakika moja kabla ya muda wa kawaida kumalizika, Arsenal ilisawazisha kupitia Olivier Giroud aliyeingia uwanjani katika kipindi cha pili cha mchuano huo.
Hii ndio mara ya kwanza tangu mwaka 1992 kwa Manchester United kutoka sare mara tatau mfulilizo na Arsenal katika uwanja wake wa nyumbani.
Sare hii ya Arsenal inaifanya kutopata ushindi katika uwanja wa Old Trafford kwa muda wa miaka 10 iliyopita, na kocha wa Arsenal Arsene Wenger bado hajafanikiwa kumshinda Jose Mourihno katika michuano 12 walizocheza.
Arsenal kwa sasa inashikilia nafasi ya tatu kwa alama 25 huku Manchester United ikiwa ya sita kwa alama 19.
Kikosi cha Arsenal: Petr Cech, Carl Jenkinson, Shkodran Mustafi, Laurent Koscielny, Nacho Monreal, Francis Coquelin, Mohamed Elneny, Theo Walcott, Mesut Özil, Aaron Ramsey, Alexis Sánchez
Wachezaji wa akiba : David Ospina, Gabriel, Kieran Gibbs, Alex Iwobi, Alex Oxlade-Chamberlain, Granit Xhaka, Olivier Giroud
Kikosi cha Manchester United : David de Gea, Antonio Valencia, Phil Jones, Marcos Rojo, Matteo Darmian, Michael Carrick, Ander Herrera, Juan Mata, Paul Pogba, Anthony Martial, Marcus Rashford
Wachezaji wa akiba : Sergio Romero, Daley Blind, Morgan Schneiderlin, Jesse Lingard, Ashley Young, Memphis Depay, Wayne Rooney
Tathmini fupi kuhusu timu hizi mbili kabla ya mchuano wa Jumamosi:
Kufikia mchuano wa leo Manchester United ilikuwa imefungwa mara moja tu na Arsenal katika michuano 10 iliyopita, ambapo mwaka 2015 Arsenal ikicheza nyumbani ilipata ushindi wa mabao 3-0.
Kwa michuano 10 iliyopita, Manchester United imeshinda mara 6 na kutoka sare mara 3 na Arsenal.
Hata hivyo, Arsenal kwa muda wa mechi 10 zilizopita, haijapata ushindi wowote katika uwanja wa Old Trafford, mara ya mwisho ikiwa ni ushindi wa mwaka 2006.
Michuano miwili iliyopita ambayo Manchester United imecheza nyumbani imetoka sare na Arsenal.