Mourinho asema wachezaji wake wana presha, ajipanga kufanya vizuri mechi zijazo
Mashabiki wa klabu ya Manchester United ya nchini Uingereza, wanaendelea kujiuliza kuhusu matokeo mabaya ambayo timu yao imeandikisha mwishoni mwa juma, wakati wa mchezo wa ligi kuu ya nchini Uingereza.
Imechapishwa:
Kipigo cha mabao 3-1 kutoka kwa klabu ya Watford kwenye mchezo wa ligi kuu, kiliongeza sintofahamu kuhusu mustakabali wa timu hiyo na kocha wake mpya Jose Mourinho, ambaye ameshuhudia timu yake ikipata kipigo cha tatu mfululizo.
Kipigo cha mwishoni mwa juma kilifuatia kile cha katikati ya wiki iliyopita dhidi ya Feyenoord cha bao 1-0 kwenye mchezo wa kombe la Europa League na kabla ya hapo ilipokea kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa klabu ya Manchester City katika mchezo wa ligi kuu ya Uingereza.
Kocha mkuu wa klabu hiyo, Jose Mourinho, akizungumza baadaya mchezo wa timu yake dhidi ya Watford, amesema kuwa kufungwa kwa timu yake kumetokana na wachezaji wake kuwa kwenye shinikizo kubwa la kucheza kwenye timu ambayo imeshatwaa taji la ligi kuu kwa mara 20.
“Baadhi ya wachezaji wanashinikizo na kujiona wanawajibu mkubwa zaidi,” alisema kocha Jose Mourinho.
“Tulianza msimu wetu vizuri sana. Lakini je nilifikiria kuwa timu yangu iko tayari, imara na isifungwe? La hasha.” aliongeza kocha Jose Mourinho.
Kocha Jose Mourinho tayari ameshapoteza michezo mitatu mfululizo toka kuanza kwa msimu wa mwaka huu ikiwa ni mara ya kwanza toka mwezi February 2002, wakati akiwa kocha mkuu wa klabu ya FC Porto.
Manchester United imeshinda taji ngao ya jamii pamoja na mechi zake tatu za mwanzo za ligi kuu ikiwa chini ya kocha Jose Mourinho, ambaye aliziba nafasi ya kocha Louis van Gaal.