Mitchel Platini asema hajutii kupokea Dola Milioni 2 kutoka kwa Blatter
Aliyekuwa rais wa Shirikisho la soka barani Ulaya UEFA Michel Platini, amesema hajutii kupokea Dola Milioni 2 kutoka kwa aliyekuwa rais wa Shirikisho la soka duniani FIFA Sepp Blatter kama malipo ya kazi ya ushauri aliyomfanyia.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Platini mwenye umri wa miaka 62 amesisitiza kuwa anaamini hakufanya kosa lolote licha ya kupigwa marufuku ya kutoshiriki katika maswala ya soka kwa miaka minne.
Raia huyo wa Ufaransa ametoa kauli hiyo baada ya kuhudhuria mkutano mkuu wa UEFA jijini Athens nchini Ugiriki.
Kamati ya nidhamu ya FIFA, ilimpa adhabu Platini na Blatter kwa madai kuwa fedha hizo hazikutolewa kwa utaratibu uliowekwa, madai ambayo wawili hao wameendelea kuyakanusha.
Platini amewaambia wadau wengine wa soka kuwa anawatakia mema wanapoendeleza gurudumu la soka bila ya uwepo wake.
Atakumbukwa kuwa mchezaji wa zamani wa timu ya taifa ya soka ya Ufaransa, lakini pia kushinda taji la mchezaji bora duniani mara tatu na kuwa rais wa sita wa UEFA kati ya mwaka 2007 hadi 2015.
Platini ambaye amewahi kuwa Naibu rais wa FIFA, aliwahi kuwania urais wa Shirikisho hilo lakini akajiondoa kwa sababu ya tuhma za ufisadi dhidi yake.