Blatter awasilisha rasmi rufaa yake CAS, sasa kusubiri hatma yake
Aliyekuwa wakati fulani rais wa shirikisho la mpira wa miguu duniani, FIFA, Sepp Blatter, Alhamisi ya juma hili amerejea tena mahakamani katika jaribio lake la mwisho kujaribu kupindua uamuzi wa kufungiwa kujihusisha na masuala ya soka kwa muda wa miaka 6 kufuatia kashfa ya rushwa.
Imechapishwa:
Blatter amewasilisha pingamizi lake la mwisho ambapo katika juhudi za kujaribu kusafisha jina lake katika mahakama ya kimataifa ya michezo duniani, CAS, akitaka kubatilishwa kwa uamuzi wa kamatik ya maadili ya FIFA.
Blatter ambaye tayari amesema adhabu aliyopewa ni “ujinga” aliwasili kwenye mahakama ya CAS iliyoko Lausanne, kujaribu kuwashawishi majaji wa mahakama hiyo kutengua adhabu ya kufungiwa miaka 6.
Kesi hiyo iliyowasilishwa na Blatter itasikilizwa kwa siku moja, lakini uamuzi wake huenda ukachukua majuma kadhaa kabla ya kiongozi huyo kujua hatma yake.
Juma lililopita Blatter alinukuliwa akisema kuwa bado ana imani na mahakama ya CAS.
Sintofahamu kwenye utawala wa soka wa Blatter ulianza baada ya vyombo vya usalama nchini Uswisi kudai vinamchunguza yeye pamoja na viongozi wengine wa FIFA kwa tuhuma za rushwa ya dola za Marekani milioni 2, wakati alipoidhinisha kupewa rafiki yake wa karibu, Michel Platini.
Tuhuma hizi zilisababisha asimamishwe kwa muda na kamatik ya maadili ya FIFA, ambapo baadae uchunguzu wa ndani uliofanywa na vyombo huru vya FIFA ulibaini kiongozi huyo kukiuka miiko ya uongozi na kufungiwa kwa miaka nane kabla ya kukata rufaa na kupunguziwa adhabu hiyo hadi miaka 6.
Jaribio la Blatter huenda likashindikana kutokana na ukweli kuwa jaribio la rafiki yake Michel Platin katika mahakama hiyo kutaka uamuzi wa kufungiwa miaka 6 nae ubatilishwe, kugonga mwamba.