Niyonsaba aishindia Burundi medali ya fedha huku Semenya akishinda dhababu mbio za Mita 800
Francine Niyonsaba ameishindia nchi yake ya Burundi medali ya fedha katika mbio za Mita 800 kwa upande wa wanawake katika Michezo ya Olimpiki inayokamilika Jumapili nchini Brazil.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Niyonsaba mwenye umri wa miaka 23, alimaliza katika nafasi ya pili kwa muda wa dakika 1 sekunde 56 nukta 49.
Hii ndio medali ya pili kwa nchi ya Burundi, tangu mwaka 1996 wakati Michezo ya Olimpiki ilipoandaliwa mjini Atlanta nchini Marekani na Venuste Niyongabo kushinda medali ya dhahabu katika mbio za Mita 5000 kwa upande wa wanaume.
Niyonsaba ambaye amekuwa akishikilia rekodi ya taifa nchini mwake kwa muda wa dakika 1 sekunde 58 nukta 67, ameweka muda bora katika Michezo hii.
Nafasi ya kwanza, katika mbio hizi ilimwendea Caster Semenya rais wa Afrika Kusini mwenye umri wa miaka 25, ambaye alishinda medali ya dhahabu kwa muda wa dakika 1 sekunde 55 nukta 28.
Hii ndio medali yake ya kwanza katika Michezo ya Olimpiki baada ya kumaliza wa pili katika Michezo ya Olimpiki mwaka 2012 iliyofanyika jijini London nchini Uingereza.
Mkenya Margaret Wambui naye aliishindia nchi yake medali ya shaba baada ya kumaliza wa tatu kwa muda wa dakika 1 sekunde 56 nukta 89.
Hii ndio iliyokuwa Michezo yake ya kwanza ya Olimpiki kwa Wambui mwenye umri wa miaka 20 kushiriki, na kuweka muda bora kutoka ule wa dakika 2 nukta 44 aliyoweka wakati wa mashindano ya ndani ya dunia yaliyofanyika nchini Marekani mapema mwaka huu.